Juhudi za viongozi wa Umoja wa Afrika kuhusu mazungumzo ya kitaifa Sudan
Viongozi wa Umoja wa Afrika AU wameanzisha juhudi za kufufua mazungumzo ya kitaifa nchini Sudan ambayo yamekuwa na mwendo wa kusuasua.
Mwenyekiti wa kiduru wa Umoja wa Afrika amefanya safari nchini Sudan ambapo leo amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Omar Hassan al-Bashir wa nchi hiyo. Rais Alpha Condé ambaye ndiye Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika pamoja na mambo mengine, katika mazungumzo yake na Ris al-Bashir amejadiliana naye suala la mazungumzo ya kitaifa ya nchi hiyo.
Aidha viongozi hao wamejadili na kubadilishana mawazo kuhusiana na matukio ya kisiasa ya Sudan ambayo yamegubikwa na kivuli cha mazungumzo ya kitaifa. Taarifa zaidi zinasema kuwa, Rais Omar Hassan al-Bashir na mwenyekiti wa kiduru wa Umoja wa Afrika wamezungumzia pia masuala ya kieneo na kimataifa.
Mbali na mgogoro wa ndani, Sudan kwa sasa inakabiliwa na matatizo mengi likiwemo la kudorora uchumi wa nchi hiyo. Rais Omar al-Bashir anatuhumiwa na wapinzani kwamba, ameshindwa kuboresha hali ya mambo ya nchi hiyo likiwemo suala la uchumi.
Ikumbukwe kuwa, mwaka jana Rais Omar al Bashir wa Sudan alitangaza kuwa ataondoka madarakani mwaka 2020 na kwamba hana mpango wa kugombea tena kiti cha Urais kwa muhula mwingine.
Omar Hassan al Bashir amekuwa madarakani tangu baada ya mapinduzi ya mwaka 1989 na amechaguliwa kuwa rais mara tatu tangu wakati huo.