Wasomi 1500 wa Misri wapinga kupewa Saudia visiwa vya nchi yao
Shakhsia na wasomi 1500 wa Misri wametangaza rasmi upinzani wao kwa uamuzi wa serikali ya nchi hiyo wa kutaka kuipa Saudi Arabia visiwa viwili vya Misri vya Tiran na Sanafir.
Kwa mujibu wa mtandao wa al Quds al Arabi, shaksia na wasomi hao 1500 wamepinga hatua yoyote ya bunge au serikali ya Misri ya kudharau haki ya nchi hiyo ya kumiliki visiwa viwili vya Tiran na Sanafir na kuamua kuimega ardhi ya nchi hiyo na kuipa Saudi Arabia.
Waliotia saini taarifa ya wasomi hao ambayo imepewa jina la "hatutorudi nyuma" wamesisitiza kuwa, hakuna serikali wala chombo chochote kilicho na haki ya kulegeza kamba katika kulinda kila shibri ya ardhi ya Misri.
Wasomi hao wamelitaka bunge na serikali ya Misri kufuta makubaliano ya kuchorwa mipaka mipya baina ya nchi yao na Saudi Arabia na waheshimu uamuzi wa mahakama uliotolewa na mahakama ya juu kabisa ya Misri.
Baadhi ya duru za serikali zimetangaza kuwa, bunge la Misri limefikia uamuzi wa kuanza kujadili makubaliano ya nchi hiyo na Saudia kuhusiana na visiwa viwili vya Misri vya Tiran na Sanafir siku chache zijazo.