Nov 11, 2017 03:13 UTC
  • Polisi Nigeria yatumia mabomu kuvunja Arubaini ya Imam Hussein AS

Polisi nchini Nigeria imetumia mabomu ya gesi ya kutoa machozi kuvunja matembezi ya amani ya waumini wa Kiislamu waliokuwa wakishiriki maombolezo ya Arubaini ya Imam Hussein (AS), mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW) katika mji mkuu Abuja.

Kamisheni ya Haki za Binadamu ya Kiislamu yenye makao yake makuu mjini London, Uingereza imekosoa kitendo hicho cha kushambuliwa kwa gesi ya kutoa machozi waandamanaji hao, wakiwemo wanawake na watoto wadogo.

Moja ya picha za hujuma hiyo ya jana Ijumaa imeonyesha mtu mmoja aliyekuwa kwenye maandamano hayo akiwa amelowa damu kwenye shati lake, ingawaje haikubainika iwapo aligongwa usoni na risasi ya plastiki au kopo la bomu la gesi ya kutoa machozi.

Aidha Jumapili ya wiki iliyopita, askari polisi wa Nigeria waliushambulia msafara wa waumini waliokuwa wakishiriki katika maombolezo ya Arubaini ya Imam Hussein AS katika jimbo la Kano, kaskazini mwa nchi na kuwaua shahidi Waislamu wawili wa madhehebu ya Shia.

Ambulensi ikibeba majeruhi jimboni Kano

Polisi ya Nigeria mbali na kuwafyatulia risasi waumini waliokuwa katika msafara huo, pia waliwavurumishia mabomu ya gesi ya kutoa machozi.

Itakumbuwa kuwa mwezi Disemba mwaka 2015 jeshi la Nigeria lilihujumua shughuli ya kidini katika mji wa Zaria na kuwaua kwa umati Waislamu zaidi ya 1,000. Katika tukio hilo Sheikh Ibrahim Zakzaky Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria akiwa na mke wake walijeruhiwa na kutiwa mbaroni na Jeshi la Nigeria, na mpaka sasa wanaendelea kuzuiliwa chini ya mazingira magumu katika mojawapo ya vituo vya kijeshi vya nchi hiyo bila kufunguliwa mashitaka. 

Tags