Rais Rouhani wa Iran amtumia salamu Rais Kabila wa DRC
Rais Hassan Rouhani wa Iran amemtumia salamu za pongezi Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa munasaba wa maadhimisho ya siku ya uhuru wa nchi hiyo.
Katika ujumbe wake huo hii leo, Rais Rouhani amempongeza Rais Kabila kwa munasaba wa kumbukumbu ya miaka 58 ya uhuru wake ilioupata kutoka kwa waliokuwa wakoloni wa taifa hilo, Ubelgiji, Juni 30 mwaka 1960.
Rais Rouhani ameelezea matumaini yake kuwa kutokana na irada ya kisiasa ya wakuu wa nchi mbili, uhusiano wa Tehran na Kinshasa unaweza kuimarika kwa kutumia uwezo uliopo.
Rais Rouhani amemtakia Rais Kabila mafanikio na ufanisi kwa watu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Taarifa zisizo rasmi kutoka Kinshasa zinasema Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo alifuta gwaride la jeshi katika maadhimisho ya uhuru kutokana na kuwepo tetesi za uasi jeshini.
Badala ya kushiriki katika gwaride la maadhimisho ya uhuru, Kabila alihutubia taifa kupitia televisheni inayomilikiwa na serikali Ijumaa usiku ambapo aliwahakikishia wananchi kuwa uchaguzi mkuu utafanyika kama ilivyopangwa na kwa usimamizi wa Tume ya Uchaguzi CENI. Vilevile ametoa wito kwa wananchi kudumisha umoja.