Jeshi la Algeria laanza oparesheni kubwa karibu na mpaka wa Tunisia
Jeshi la Algeria limeanzisha oparesheni kubwa katika maeneo ya mpaka wa pamoja na nchi jirani ya Tunisia kufuatia kutekelezwa shambulio la kigaidi Jumapili iliyopita katika mkoa mmoja ulioko mpakani wa Jendouba. Wanajeshi sita waliuawa na watatu kujeruhiwa katika shambulio hilo la kigaidi.
Duru za habari za Algeria zimearifu kuwa jeshi la nchi hiyo limeanzisha oparesheni kubwa katika mikoa mitatu ya Tabsah, Souk al Ahras na Al Oued inayopatikana katika mpaka wa pamoja na Tunisia ili kuzuia kujipenyeza magaidi katika ardhi ya Algeria.
Wanajeshi wa Algeria zaidi ya elfu mbili wanashiriki kwenye oparesheni hiyo. Wakati huo huo duru za usalama za Tunisia jana zilitangaza kuwa kundi moja la kigaidi limefanya shambulio katika mkoa wa Jendouba kaskazini magharibi mwa nchi hiyo karibu na mpaka wa Algeria. Tunisia imekuwa ikikabiliwa na wimbi la mashambulizi ya kigaidi tangu mwaka 2011. Umoja wa Mataifa umeripoti kuwa raia wa Tunisia zaidi ya elfu tano wamejiunga na makundi ya kigaidi huko Iraq na Syria.