Rais wa Msumbiji: Vikosi vya nchi vinakabiliana vikali na wanamgambo vamizi
Rais Filipe Nyusi wa Msumbiji amesema kuwa jeshi la vikosi vya ulinzi na usalama vya nchi hiyo limekabiliana vikali na wanamgambo vamizi baada ya kushambulia mji wa Macomia katika jimbo tajiri kwa gesi kaskazini mwa nchi hiyo Alhamisi iliyopita.
Mji wa Macomia unaopatikana umbali wa kilomita 230 kutoka Pemba makao makuu ya jimbo la Cabo Delgado ni mji muhimu kuwahi kushambuliwa hivi karibuni tangu kuanza mwaka huu kufuatia kushadidi mashambulizi ya wanamgambo hao wanaotajwa kuwa na mfungamano na kundi la kigaidi la Daesh.
Wachambuzi wa mambo wanasema kuwa mapigano makali yalishuhudiwa baada ya kushambuliwa mji huo. Mapigano hayo yalianza mapema Alhamisi iliyopita kufuatia hujuma ya wanamgambo hao vamizi waliohujumu nyumba za raia na miundo mbinu na kusababisha raia kuyakimbia makazi yao.
Rais Pilipe Nyusi wa Msumbiji amesema kuwa mapigano yaliyoendeshwa na vikosi vya ulinzi na usalama vya nchi yake yalikuwa makubwa na yaliyozaa matunda. Amesema wamepata taarifa kwamba makada wakuu wa wanamgambo hao wameuliwa.