Francis Wanjohi: Ash Shabab yafanya njama za kuzidi kuwadanganya vijana wa Kenya
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i7501-francis_wanjohi_ash_shabab_yafanya_njama_za_kuzidi_kuwadanganya_vijana_wa_kenya
Kamanda wa eneo la Pwani nchini Kenya amesema kuwa, kundi la ash Shabab la Somalia linaendelea na njama zake za kuwadanganya vijana wa Kenya ili wajiunga na kundi hilo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
May 21, 2016 11:28 UTC
  • Francis Wanjohi: Ash Shabab yafanya njama za kuzidi kuwadanganya vijana wa Kenya

Kamanda wa eneo la Pwani nchini Kenya amesema kuwa, kundi la ash Shabab la Somalia linaendelea na njama zake za kuwadanganya vijana wa Kenya ili wajiunga na kundi hilo.

Shirika la habari la Xinhua limemnukuu Kamanda Francis Wanjohi akisema hayo leo na kuongeza kuwa, kundi la ash Shabab linatumia mbinu mbalimbali kuwatumbukiza kwenye mtego wake vijana wa Kenya na kuwafanya watende vitendo vya uhalifu.

Amesema, katika operesheni ya karibuni kabisa, jeshi la polisi la Kenya limefanikiwa kuwatia mbaroni wanachama watano wa ash Shabab katika mji wa Wajir, wa kaskazini mashariki mwa Kenya.

Wanjohi ameongeza kuwa, jeshi la polisi limefanikiwa pia kumtia mbaroni Ramadhan Khamis Kufungwa, mmoja wa viongozi wakuu wa kundi la ash Shabab nchini Kenya.

Kundi la ash Shabab lilikuwa linadhibiti maeneo mengi ya Somalia ikiwemo sehemu kubwa ya mji mkuu Mogadishu tangu mwaka 2006 hadi 2011 wakati lilipozidiwa nguvu na kurudishwa nyuma na askari wa Umoja wa Afrika.

Kundi hilo limekuwa likifanya mashambulizi pia katika nchi jirani hasa Kenya.

Ikumbukwe pia kuwa Mombasa ni mji wa pili wenye watu wengi zaidi nchini Kenya na katika miaka ya hivi karibuni umekuwa ukilengwa na mashambulizi mbalimbali ya genge la ash Shabab.