Wizara ya Ulinzi Niger: Watu 1200 wameuawa katika mashambulio ya kigaidi
Wizara ya Ulinzi ya Niger imetangaza kuwa, kwa akali watu 1200 wameuawa nchini humo tangu mwaka 2013 hadi sasa kufuatia mashambulio mbalimbali ya kigaidi.
Taarifa iliyotolewa na Alkassoum Indatou, Waziri wa Ulinzi wa Niger inaeleza kwamba, kati ya watu 1200 waliouawa katika mashambulio hayo ya kigaidi 700 ni raia na 500 waliobakia ni askari.
Akijibu swali la mmoja wa Wabunge wa Niger baada ya kuitwa Bungeni kwamba, je Niger imechukua hatua gani kukabiliana na mgogoro wa usalama, waziri Alkassoum Indatou amebainisha kwamba, wizara yake imechukua hatua za lazima kwa ajili ya kukabiliana na harakati na hujuma za kigaidi na imepoteza askari wengi katika njia hiyo.
Aidha Waziri wa Ulinzi wa Niger amesema kuwa, hujuma za kigaidi zimetoa pigo kubwa kwa jamii ya nchi hiyo na kuwafanya raia waliokuwa wakitaabika kwa umasikini kuwa katika hali mbaya zaidi ya kukosa haki za kijamii.
Hayo yanajiri katika hali ambayo, Manispaa kadhaa za mkoa wa Maradi nchini Niger zinaathiriwa vibaya na machafuko ya magenge yaliyojizatiti kwa silaha nzito kutoka majimbo jirani ya Nigeria ya Katsina, Sokoto na Zamfara.
Kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR, mkoa wenyewe wa Maradi umewapa hifadhi wakimbizi wapatao elfu kumi kutoka Nigeria waliolazimika kuhama makazi yao kutokana na kuandamwa na mashambulio makali.
Harakati za kundi la kigaidi la Boko Haram la nchini Nigeria zimekuwa sababu pia ya ukosefu wa amani na usalama mpakani wa Niger.