Dec 11, 2022 12:40 UTC
  • Waislamu wa Nigeria waandamana kulaani ukandamizaji wa Mashia Azerbaijan

Wananchi Waislamu wa Nigeria wameandamana katika mji mkuu wa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika kulalamikia mbinyo na ukandamizaji dhidi ya Waislamu wa madhehebu ya Shia nchini Azerbaijan.

Waandamanaji hao walikusanyika jana Jumamosi katika Msikiti wa Jamia wa Abuja, ambapo walisikika wakipiga nara dhidi ya vyombo vya dola vya Azerbaijan kwa kuwanyongesha Waislamu wa Kishia hususan wafuasi wa Harakati ya Umoja wa Kiislamu (MMU).

Abdullah Musa, Katibu Mkuu wa Jukwaa la Akademia la Harakati ya Kiislamu ya Nigeria ambaye alikuwa mmoja wa waandamanaji amenukuliwa akisema, "Serikali (ya Azerbaijan) inawahukumu kiholela (Mashia) wa nchi hiyo."

Amesisitiza kuwa, Waislamu wote kote duniani wana wajibu wa kupinga dhulma na ukandamizaji unaofanywa dhidi ya Waislamu wa madhehebu ya Shia wa Azerbaijan.

Baadhi ya waandamanaji hao wa Nigeria wamesikika wakipiga nara za 'Mauti kwa Marekani' na "Mauti kwa Israel' huku wengine wakiwa wamebeba picha za Haj Taleh Baqir Zadeh, kiongozi wa Harakati ya Umoja wa Kiislamu nchini Azerbaijan (MMU).  

Maandamano kama haya yameshuhudiwa pia katika jimbo la Kano la kaskazini mwa Nigeria, ambapo Waislamu wa nchi hiyo ya Afrika Magharibi wametangaza uungaji mkono wao kwa wenzao wa Azerbaijan wanaokandamizwa.

Bango moja lilikuwa limeandikwa "Harakati ya Kiislamu ya Nigeria chini ya uongozi wa Sheikh Ibrahim Zakzaky inasimama pamoja na Haj Taleh Baqir Zadeh na ndugu wengine wanaokandamizwa Azerbaijan."

Wakati huohuo, Kamisheni ya Haki za Binadamu ya Kiislamu yenye makao makuu yake mjini London limetoa taarifa ya kulaani ukandamizaji huo unaofanya na serikali 'fisadi' ya Azerbaijan kwa kuwawekea mbinyo wanachama wa Harakati ya Umoja wa Kiislamju (MMU).

 

Tags