Machafuko yaongezeka Afrika Kusini kabla ya uchaguzi wa mabaraza ya miji
Machafuko yameongezeka nchini Afrika Kusini sanjari na kukaribia uchaguzi wa mabaraza ya miji nchini humo.
Machafuko hayo ambayo yalianza miezi kadhaa iliyopita, yameripotiwa kuongezeka mjini Pretoria hivi karibuni.
Magari kadhaa yalichomwa moto wakati watu walipokuwa wakipinga kuwasili eneo la tukio mmoja wa wagombea ambapo pia walifunga njia.
Aidha mmoja wa viongozi wa chama tawala cha ANC ameuawa katika moja ya mikutano ya kampeni. Weledi wa mambo wanaelezea matatizo ya ndani ya chama cha ANC na pia tuhuma zinazomkabili Rais Jacob Zuma, kuwa ndiyo sababu itakayokifanya chama hicho kupoteza viti vingi katika uchaguzi wa mabaraza ya miji.
Ikumbukwe kuwa, Mahakama ya Katiba ya Afrika Kusini ilitoa hukumu ikimtaka rais huyo kurejesha Euro milioni 20 alizozichota kutoka Hazina kwa ajili ya ukarabati wa nyumba yake binafsi.