Jul 21, 2023 07:57 UTC
  • Iran: Mkuu wa UN achukue msimamo mkali dhidi ya kuvunjiwa heshima Qurani

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amemuandikia barua Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, akimtaka achukue msimamo mkali dhidi ya vitendo vya kuvunjiwa heshima Qurani Tukufu.

Hossein Amir-Abdollahian alimuandikia Guterres barua hiyo jana Alkhamisi, saa chache baada ya kafiri Salwan Momika kwa mara nyingine tena kuivunjia heshima Qur'ani Tukufu chini ya ulinzi kamili wa polisi wa Sweden mjini Stockholm.

Barua hiyo imesema, kitendo hicho cha kudhalilisha matukufu ya kidini si tu kimewakasirisha na kuumiza hisia za Waislamu kote duniani, lakini pia wafuasi wa dini tukufu kote ulimwenguni.

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi ya juu wa Iran amemkumbusha Katibu Mkuu wa UN kwenye barua hiyo kuwa, lengo la vitendo hivyo vya kuvunjia heshima matukufu ya Kiislamu ni kuendeleza wimbi la vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu, na kushajiisha misimamo mikali.

Sehemu nyingine ya barua hiyo imesema, hatua ya serikali ya Sweden ya kutoa kibali cha kufanyika mkusanyiko kwa ajili ya kuivunjia heshima Qur'ani Tukufu mjini Stockholm ni kuchupa mistari myekundu ya Waislamu na kwamba serikali ya Sweden inapaswa iombe radhi kwa jinai hiyo.

Kafiri Salwan Momika kabla ya kuidhalilisha Qurani Tukufu

Jana Alkhamisi, raia wa Sweden mwenye asili ya Iraq, Salwan Momika kwa mara nyingine tena aliivunjia heshima Qur'ani Tukufu chini ya ulinzi kamili wa polisi wa Sweden mjini Stockholm.

Kafiri huyo mara hii alikanyaga na kupiga mateke nakala ya Kitabu hicho kitukufu cha Waislamu nje Msikiti mkuu mjini Stockholm, karibu na ubaloi wa Iraq. Ikumbukwe kuwa, Juni 28 wakati wa sikukuu ya Idul Adh'ha, Momika (37) aliidhalilisha Qurani Tukufu kwa kuichana na kuchoma moto.

Ulimwengu wa Kiislamu umelaani vikali wimbi hilo la vitendo viovu vya kuvunjiwa heshima Qurani Tukufu huko nchini Sweden kwa ridhaa ya serikali ya Stockholm. 

Tags