Ebrahim Raisi: Palestina ni kadhia ya kwanza ya ulimwengu
Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, Palestina imegeuka na kuwa kadhia ya kwanza ulimwengu wa mwanadamu.
Ebrahim Raisi amesema hayo leo hapa mjini Tehran katika Kongamano la Kimataifa la Kimbunga cha al-Aqswa na Kuamsha Hisia za Ubinadamu za Walimwengu na kueleza kwamba, Imam Khomeini (RA), muasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alisema kuwa, Palestina ni suala la kwanza la ulimwengu wa Kiislamu, na kukombolewa Quds ni jambo la kipaumbele katika ulimwengu wa Kiislamu.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa, muqawama, mapambano na kusimama kidete mkabala wa adui Israel ndio suluhisho la kadhia ya Palestina na kuongeza kuwa: "Ikiwa mkondo wa kidhalimu hauelewi lugha ya mantiki na mazungumzo, basi mantiki pekee ni muqawama na mapambano."
Kadhalika Sayyid Ebrahim Raisi amesema, katika sera za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, suala la kuunga mkono kadhia ya Palestina na makundi ya muqawama na mapambano ni miongoni mwa ajenda za taifa hili.
Aidha amehoji kwa kusema, hivi tunaweza kuwapuuza watu wanaodhulumiwa zaidi duniani? Ni lazima kumuunga mkono na kumtetea mtu ambaye anasimama na kujitetea yeye, dini na familia yake.
Vilevile Rais wa Jamahuri ya Kiislamuu ya Iran amesema katika kongamano hilo la Kimataifa la Kimbunga cha al-Aqswa na Kuamsha Hisia za Ubinadamu za Walimwengu kwamba, uvamizi wa Israel na ukaliaji wake kimabavu ardhi za Wapalestina unapaswa kukomeshwa na wakati huo huo mvamizi aadhibiwe na kulipa fidia.
Vilevile amesema, kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala bandia wa Israel hakudhamini kwa namna yoyote ile usalama wa Asia Magharibi wala wa utawala haramu wa Israel.