Iran na Sudan zatilia mkazo kuiunga mkono Palestina
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan wameisitiza ulazima wa kuliunga mkono taifa la Palestina mkabala wa utawala wa Kizayuni wa Israel.
Pande mbili hizo zimebainisha haya pambizoni mwa Mkutano wa Jumuiya ya NAM huko Kampala Uganda.
Muhammad Mokhber Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Ali al Sadiq Ali Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan jana walikutana na kuzungumza pambizoni mwa Mkutano wa Jumuiya ya Nchi Zisizofungamana na Siasa za Upande Wowote (NAM) huko Kampala mji mkuu wa Uganda.
Katika mazungumzo hayo, Mokhber amesema serikali na wananchi wa Iran wana hamu ya kuendeleza uhusiano wa kisiasa na wenzao wa Sudan na kusisitiza kuwa, nchi mbili zina msimamo wa pamoja kuhusu suala la kuwatetea wananchi madhulumu wa Palestina. Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia amezitolea wito nchi za Kiislamu kuzidisha juhudi za kusitisha jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya wananchi madhulumu wa Ukanda wa Gaza.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Sudan pia amesema kukatwa uhusiano wa kisiasa kati ya nchi mbili hizi mwaka 2015 halikuwa takwa la serikali na watu wa Sudan na akasisitiza kuwa serikali ya Sudan inafanya juhudi ili kuhuisha uhusiano na Iran.