Rais Masoud Pezeshkian: Kuimarisha umoja na mshikamano lengo kuu la safari yangu nchini Iraq
(last modified Sat, 14 Sep 2024 07:18:22 GMT )
Sep 14, 2024 07:18 UTC

Rais Masoud Pezeshkian wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema umoja na mshikamano ni lengo kuu la safari yake nchini Iraq na kuongeza kuwa nia na azma ya serikali za Tehran na Baghdad ni kuimarisha uhusiano wa pande mbili na ushirikiano wa kieneo.

Pezeshkian, baada ya kurejea kutoka Iraq, amesisitiza juu ya kufuatilia malengo ya safari hiyo kuhusu umoja na mshikamano wa nchi mbili. Amesema kuhusu masuala ya uhusiano wa kisiasa, kiuchumi, kiutamaduni na kiusalama, amejadiliana na Rais, Waziri Mkuu, Spika wa Bunge, Mkuu wa Vyombo vya Mahakama na wa vyama vya siasa vya Iraq na kuwafahamisha mtazamo wa serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kuhusu masuala hayo.

Rais Pezeshkian amesema katika safari yake nchini Iraq, hati 14 za maelewano na ushirikiano wa nchi mbili zimetiwa saini, na kuwa kilicho muhimu zaidi ni kwamba ili kufikia lugha moja, timu kutoka pande mbili inapaswa kubuni mipango ya muda mrefu ambayo itasainiwa wakati muwafaka.

Rais Masoud Pezeshkian akiwa safarini mjini Baghdad

Rais Pezeshkian ameongeza kuwa katika kikao na Wairani wanaoishi Iraq, masuala ya kiuchumi, pamoja na kurahisisha usafiri wao ndani na nje ya nchi yalijadiliwa na kuamuliwa kuwa matatizo yaliyopo yatauliwe kwa msingi sera jumla za mfumo wa Kiislamu.

Jumatano asubuhi tarehe 11 September, Rais Masoud Pezeshkian wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, katika safari yake ya kwanza nje ya nchi, aliwasili Baghdad mji mkuu wa Iraq, akiongoza ujumbe wa ngazi za juu wa kisiasa na kiuchumi na kulakiwa rasmi na Waziri Mkuu wa Iraq, Mohammad Shia as-Sudani.

Lengo kuu la safari ya Pezeshkian mjini Baghdad, lilikuwa ni kuimarisha uhusiano wa pande mbili ambapo safari hiyo imekisiwa pakubwa na vyombo vya habari vya Iraq, kieneo na kimataifa.

Tags