Kulegeza msimamo Marekani kuhusiana na shambulio la kijeshi dhidi ya Iran
Rais Donald Trump wa Marekani iwe ni katika kipindi cha kampeni zake za uchaguzi au baada ya kuingia katika ikulu ya White House Januari 2017, amechukua mkondo wa siasa za kutaka kuudhoofisha na kuuangusha mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Washington ikiwa katika fremu ya kutekeleza siasa za mashinikizo kadiri inavyowezekana, imeanzisha vita vya kiuchumi dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na wakati huo huo, katika wiki za hivi karibuni ilitoa vitisho vya kijeshi dhidi ya Tehran.
Pamoja hayo, radiamali kali ya Iran ya kuwa tayari kukabiliana na aina yoyote ya shambulio na vile vile upinzani mkubwa dhidi ya siasa za Trump mkabala na Iran nje na ndani ya Maarekani, na hata kutoka kwa washirika wa Ulaya wa Washington ni mambo ambayo yameifanya serikali ya Trump ilegeze kamba na kuachilia mbali madai yake ya hapo awali.
Katika uwanja huo, jarida la wiki la Marekani la Time sanjari na kubainisha kwamba, Washington haina mpango wowote wa kuishambulia kijeshi Iran limeandika: Maafisa wa kijeshi wa Pentagon wanaamini kuwa, shambulio kama hilo linahitaji mipango na maandalizi ya miezi kadhaa kabla ya kutekelezwa kwake.
Ripoti ya jarida la Time ya tarehe 18 Mei inaonyesha kuwa, kwa mtazamo wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani Pentagon ni kuwa, itawezekana kuzungumzia uwepo wa 'mpango wa kijeshi' pale mpango wa shambulio au vita unapokuwa umekabidhiwa kwa Rais, na kinyume na hivyo yote yanayozungumziwa kuhusiana na hilo ni dhana na tetesi tupu.
Jarida la Time limeandeika: Maafisa watatu wa kijeshi wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani Pentagon ambao ni amilifu katika katika kuandaa mipango na kusimamia vikosi vya Marekani katika eneo la Mashariki ya Kati wamesema kuwa, hakuna mpango wa kweli na wa kutekelezeka au kitu kinachoshabihaiana na hicho kwa ajili ya kutuma kikosi kikubwa cha kijeshi katika eneo la Ghuba ya Uajemi.
Katika kipindi cha wiki mbili zilizopita, viongozi wapenda vita wa serikali ya Donald Trump yaani John Bolton, Mshauri wa Usalama wa Taifa na Mike Pompeo, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani walidai kuwa, Iran na washirika wake wanataka kuvishambulia vikosi vya Marekani na maslahi ya Washington katika eneo na wakatahadharisha kwamba, hatua hiyo itakabiliwa na radiamali kali ya Washington.
Bolton alidai kwamba, Marekani haina mpango wa kuingia vitani na Iran, lakini imejiandaa kikamilifu kutoa jibu la shambulio la aina yoyote ile kutoka kwa vikosi vya Tehran. John Bolton na Mike Pompeo wanadhani kwamba, vitisho vya kijeshi dhidi ya Iran vitaifanya Tehran ibadilishe misimamo yake na hivyo kuifanya isifanye harakati katika fremu ya kulinda maslahi yake ya kitaifa na kiusalama.
Pamoja na hayo, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imesisitiza mara chungu nzima kwamba, itatoa jibu kali kwa tishio lolote la kijeshi na uvamizi tarajiwa wa Marekani au washirika wake katika eneo. Filihali ripoti na habari mbalimbali zinaonyesha kuwa, Marekani imelegeza kamba na kubadilisha msimamo wake wa hapo awali wa tishio la kijeshi dhidi ya Iran.
Gazeti la New York Times limeripoti kuwa, Donald Trump amemwambia Patrick Shanahan, Kaimu Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo kwamba, hataki kuingia katika vita na Iran. Gazeti hilo linaongeza kuwa, katika kikao cha siku ya Jumatano tarehe 15 Mei kuhusiana na Iran, Trump alisisitiza msimamo wake juu ya suala hili kwamba, hataki kuingia katika vita na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Inaonekana kuwa, viongozi waandamizi wa Marekani filihali wamediriki kuliko wakati mwingine wowote ule hatari kubwa ya kuingia vitani na Iran na ndio maana wanafanya juhudi za kuhallisha au kubadilisha vitisho vya hapo kabla vya kutaka vita vilivyotolewa na serikali ya Donald Trump. Hii ni katika hali ambayo, msimamo wa Iran daima ni kuwa, imejiandaa kukabiliana na aina yoyote ya uvamizi wa kijeshi.
Hamid Baeidinejad, balozi wa Iran nchini Uingereza amesisitiza kuwa, kama Marekani inafuatilia hatua zisizo na dharura na kufanya uchochezi zaidi, basi sisi tuko tayari kukabiliana na nchi hii. Sisi hatufuatilii suala la kuanzisha vita, lakini taifa la Iran limejiandaa kikamilifu kwa ajili ya kusimama kidete na kukabiliana na Marekani.