Rais Rouhani: Marekani imeshindwa na kufeli mbele ya taifa la Iran
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i55124-rais_rouhani_marekani_imeshindwa_na_kufeli_mbele_ya_taifa_la_iran
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, mwaka jana maadui wa taifa la Iran walidai kuwa wanaweza kuuondoa madarakana mfumo wa Kiislamu unaotawala Iran, kuvunja uhuru wake na kuweka hatamu za nchi hiyo katika mikono ya White House, lakini hawakujua kwamba taifa la Iran litashinda na kuzima mashinikizo ya adui.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Aug 01, 2019 08:02 UTC
  • Rais Rouhani: Marekani imeshindwa na kufeli mbele ya taifa la Iran

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, mwaka jana maadui wa taifa la Iran walidai kuwa wanaweza kuuondoa madarakana mfumo wa Kiislamu unaotawala Iran, kuvunja uhuru wake na kuweka hatamu za nchi hiyo katika mikono ya White House, lakini hawakujua kwamba taifa la Iran litashinda na kuzima mashinikizo ya adui.

Rais Rouhani ameyasema hayo mapema leo wakati wa uzinduzi wa mradi mkubwa wa gesi katika eneo la Haris mkoani Azarbaijan Mashariki na kuongeza kuwa, vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran ni sawa na kushindwa kimaadili, kisiasa na kisheria kwa Wamarekani. Amesema kuwa vikwazo hivyo ni pigo na kushindwa Marekani mbele ya jumuiya za kimataifa, Umoja wa Mataifa na taifa kubwa la Iran. 

Rais Rouhani amevitaja vikwazo vya Marekani dhidi ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran kuwa ni hatua ya kitoto na kuongeza kuwa: Maadui wa taifa la Iran wamefeli na kushindwa kwa kadiri kwamba, sasa wameamua kumuwekea vikwazo Waziri wa Mambo ya Nje na kuonesha jinsi wanavyoogopa mantiki na mahojiano ya mwanadiplomasia shujaa kama Muhammad Javad Zarif. 

Rais Hassan Rouhani

Rais Hassan Rouhani amesema matokeo ya vikwazo hivyo vya Marekani dhidi ya taifa la Iran ni kuimarika zaidi na kuwa na misimamo huru na ya kujitegemea katika siasa na sekta ya viwanda ya Iran. Ameongeza kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran itaendeleza njia yake ya ustawi na maendeleo na itafika siku maadui watajutia vikwazo vyao. 

Itakumbukwa kuwa mapema leo Alkhamisi kwa wakati wa Tehran, Wizara ya Fedha ya Marekani imeendeleza uraibu wa nchi hiyo wa kuziwekea vikwazo nchi mbalimbali kwa kuliweka jina la Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika orodha ya watu waliowekewa vikwazo na nchi hiyo.