Abdollahian: Uhusiano wa Iran na Algeria upo katika mkondo sahihi
Hossein Amir Abdollahian Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema leo katika mkutano na waandishi wa habari hapa Tehran akiwa pamoja na mwenzake wa Algeria Ahmed Attaf kuwa uhusiano wa Iran na Algeria upo katika mkondo sahihi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amepongeza mkutano wa Kamisheni ya Pamoja ya nchi mbili katika ngazi ya Makamu wa Rais na Waziri Mkuu na kuashiria pia makubaliano yaliyofikiwa na Iran na Algeria ya kustawisha ushirikiano katika nyanja za sayansi, teknolojia, kilimo, madawa, viwanda na madini.
Akifafanua kuhusu masuala ya kikanda, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema Algeria haijaruhusu utawala wa Kizayuni kuwa mwanachama mtazamaji ndani ya Umoja wa Afrika (AU). Amesema siku zote Algeria imekuwa ikiiunga mkono Palestina na imekuwa na mchango muhimu katika kurejea Syria katika Jumuiya ya Nchi za Kiarabu (Arab League).
Katika mazungumzo hayo na waandishi wa habari hapa Tehran, Waziri wa Mambo ya Nje wa Algeria pia amepongeza mazungumzo ya Tehran kuhusu maendeleo ya haraka ya kikanda na kimataifa. Ahmed Attaf ameongeza kuwa uhusiano kati ya nchi mbili ni mkubwa na kwamba uhusiano huu unaweza kupelekea kupanuliwa zaidi uhusiano katika nyanja za kiuchumi.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran amesema amejadili na mwenzake wa Algeria kuhusu vita vya Ukraine, kadhia ya Palestina na hali ya mambo huko Yemen na Libya.