Wazayuni wauvamia tena Msikiti wa Al Aqsa kwa siku ya nne mfululizo
Kundi kubwa la walowezi wa Kizayuni leo wameuvamia tena kwa siku ya nne mtawalia Msikiti wa Al-Aqsa huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu huku wakilindwa na kusindikizwa na askari wa utawala haramu wa Kizayuni wa Israel.
Msikiti wa Al-Aqsa unajulikana kuwa nembo kuu ya utambulisho wa Kiislamu na Palestina ya Baitul Muqaddas (Jerusalem) na utawala dhalimu wa Israel unafanya kila njia ili kuifuata athari hiyo muhimu, lakini kusimama imara na kuwa macho wananchi wa Palestina kumeufanya utawala huo ghasibu ugonge mwamba na kushindwa kufikia lengo lake hilo ovu.
Kwa mujibu wa Chaneli ya Al-Aqsa, Idara ya Wakfu ya Quds imetangaza kuwa, mapema leo walowezi 100 wa Kizayuni waliingia katika ua wa Msikiti wa Al-Aqsa na kufanya ibada yao ya Talmudi huku wakilindwa na kusindikizwa na askari wa utawala haramu wa Kizayuni.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, katika upande mwingine askari wa utawala wa Kizayuni leo wamevamia maeneo mbalimbali ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan na kuwatia mbaroni raia watano wa Palestina.
Siku ya Jumamosi pia, kwa kutumia kisingizio cha kufanya hafla na ibada za Talmud na huku wakipewa ulinzi mkubwa na vikosi vya usalama, Wazayuni walivamia eneo la Soko la al-Qatanin karibu na Msikiti wa Al-Aqsa.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, askari wa Kizayuni waliwalazimisha wafanyabiashara Wapalestina wafunge maduka yao.../