Sayyid Hassan Nasrullah: Hizbullah kamwe haiiogopi Israel wala Marekani
Sayyid Hassan Nasrullah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Mapambano ya Hizbullah ya Lebanon amesema kuwa, muqawama hauuogopi utawala haramu wa Kizayuni wa Israel wala shetani mkuu Marekani.
Sayyid Hassan Nasrullah aliyasema hayo jioni ya jana kwa mnasaba wa kumbukumbu ya kuuawa shahidi makamanda na viongozi wa harakati hiyo ya muqawama, kupongeza mapambano ya Imamu Ruhullah Khomeini, (MA) Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kutoa mkono wa kheri na fanaka kwa Kiongozi Muadhamu Sayyid Ali Khamenei na wananchi wa lran kwa mnasaba wa ushindi wa mapinduzi ya Kiislamu ya Iran.
Akizungumzia mapambano ya makamanda wa harakati hiyo akiwemo, Sayyid Abbas Musawi, Sheikh Raghib Harb na Imad Mughniyah, amesema kuwa shakhsia hao walijitolea nafsi zao kwa ukweli na subira ya hali ya juu katika kukabiliana na adui Mzayuni.
Aidha amezungumzia nafasi hasi ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel katika eneo la Mashariki ya Kati na kufafanua kuwa hivi sasa chokochoko za Israel dhidi ya Hizbullah, zimeshtadi na kwamba Tel-Aviv inaiona harakati hiyo kuwa ni tishio nambari moja dhidi yake na kwamba, hali hiyo inautia zaidi fakhari muqawama. Sayyid Hassan Nasrullah amesema kuwa, vitisho ambavyo vimekuwa vikitolewa na utawala huo dhidi ya muqama, sio vipya na kwamba kutokana na Israel kushindwa kukabiliana na wanamuqawama, sasa inakusudia kuzidisha mashinikizo dhidi ya raia wa Lebanon ili waichukie harakati hiyo ya Kiislamu.
Katibu Mkuu wa Harakati ya Kiislamu ya Hizbullah nchini Lebanon amefafanua kuwa, hata kama Rais Donald Trump wa Marekani atampa ruhusa au kumshawishi Netanyahu, Waziri Mkuu wa Utawala Haramu wa Kizayuni wa Israel, ili kuishambulia Lebanon, suala hilo haliwezi kuutia wasi wasi muqawama. Amebainisha kwamba, hadi sasa zipo nchi kadhaa za Kiarabu ambazo zipo tayari kuulipia utawala wa Israel gharama za kuishambulia kijeshi Lebanon na kwamba ushahidi wa hilo ni uungaji mkono mkubwa wa nchi hizo za Kiarabu kwa utawala huo ghasibu katika vita vya mwaka 2006 na kwamba, hii leo pia nchi hizo zimejiandaa kwa hilo.
Sayyid Hassan Nasrullah amesema kuwa, uwezo wa muqawama na raghba yake ni msimamo thabiti wa Rais Michel Aoun wa Lebanon na kwamba, msimamo wa kiongozi huyo ndio umeizidishia uwezo na uimara harakati hiyo na kwamba, wakati wowote adui atakapohisi kuwa Hizbullah imedhoofika, basi hatosita kuishambulia Lebanon ili kufikia malengo yake haramu katika eneo.