Israel yaendeleza jinai zake dhidi ya raia wanaodhulumiwa wa Wapalestina
Utawala wa Kizayuni wa Israel umewapa amri wanajeshi wake wavamie na kuvunja makumi ya nyumba za wananchi wa Palestina katika kijiji cha Khan al Ahmar, mashariki mwa mji wa Quds unaokaliwa kwa mabavu na Wazayuni.
Gazeti la Kizayuni la Haaretz limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, meya Muisraeli wa mji wa Quds ametoa amri ya kuvunjwa nyumba za Wapalestina katika kijiji hicho na kutishia kuwa atatekeleza mpango huo katika kipindi cha wiki moja ijayo.
Wapalestina wa kijiji cha Khan al Ahmar wanaishi katika umaskini mkubwa kutokana na ukandamizaji wa utawala wa Kizayuni. Viongozi makatili wa Israel wanafanya njama za kila namna kuwapokonya Wapalestina kijiji chao hicho ikiwa ni pamoja na kuwafungia suhula zote hata za maisha ya chini kabisa. Kijiji hicho ni muhimu kwa utawala wa Kizayuni kutokana na kwamba kiko karibu na njia zinazoelekea kwenye vitongoji vya walowezi wa Kizayuni.
Dunia nzima inalalamikia siasa za utawala wa Kizayuni za kuwapora ardhi Wapalestina, kuwavunjia nyumba zao, kuwafanya wakimbizi na kuteka ardhi zao.
Hata hivyo utawala huo pandikizi unaendelea kukaidi kilio cha walimwengu kutokana na uungaji mkono wa kila upande wa madola ya kibeberu hususan Marekani.
Utawala wa Kizayuni wa Israel unaendelea kupora ardhi za Wapalestina na kujenga vitongoji vya walowezi wa Kizayuni licha ya kwamba tarehe 23 Disemba 2016, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipasisha azimio la kupinga ujenzi wa vitongoji vya walowezi hao waliokusanywa kutoka maeneo mbalimbali ya dunia na kupandikizwa kwenye maeneo waliyoporwa Wapalestina.