Uhusiano wa kibiashara wa Iran na Oman wazidi kuimarika
Naibu wa Mkuu wa Shirika la Ustawi wa Kibiashara la Iran anayehusika na masuala ya Kiarabu na Kiafrika amesema kuwa, uhusiano wa kibiashara baina ya Tehran na Muscat Oman umeimarika sana katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.
Shirika la habari la IRIB limemnukuu Mehrdad Fallah akisema hayo leo na kuongeza kuwa, kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, kiwango cha bidhaa za Iran zilizosafirishwa nchini Oman mwaka 2016 kiliongezeka kwa asilimia 42 ikilinganishwa na mwaka wa kabla yake wa 2015.
Ameongeza kuwa, kiwango cha usafrishaji bidhaa za Iran nchini Oman mwaka 2015 kilikuwa no dola milioni 376 ambapo mwaka mwaka 2016 kiliongezeka kwa dola milioni 157 na kufanya kiwango cha bidhaa za Iran zilizosafirishwa nchini Oman mwaka 2016 kuwa na thamani ya dola milioni 533.
Sehemu kubwa ya bidhaa za Iran zinazotumwa nchini Oman ni pamoja na wanyama hai, bidhaa zinazotokana na chuma, feleji, chuma cha pua, lami na shaba.
Bidhaa muhimu zaidi zinazoingizwa nchini Iran kutoka Oman ni pamoja na pikipiki, dawa n.k.