Assad ataka Waislamu waungane dhidi ya ugaidi
-
Kongamano la Kiarabu na nchi za Kiislamu
Rais Bashar al Assad wa Syria amewataka Waislamu wote duniani kuwa kitu kimoja na kuendesha mapambano dhidi ya ugaidi unaotishia eneo na ulimwengu mzima kwa ujumla. Rais Assad ameyatamka hayo katika mkutano wa wanachama wa sekretariati kuu ya Kiarabu na Jukwaa la Kiislamu kwa ajili ya kuunga mkono muqawama uliofanyika mjini Damascus Syria.
Rais wa Syria amesema kuna udharura kwa Waislamu kote ulimwenguni kuonyesha jitihada zao za dhati ili kuzuia kuenea kwa ugaidi. Rais Bashar al Assad amesisitiza pia umuhimu wa mikutano na taasisi kama hizo katika kuzidisha ufahamu na kuzuia njama za madola ya magharibi, zenye lengo la kuzikandamiza nchi za Kiarabu. Wawakilishi kutoka nchi 28 waliohudhuria kongamano hilo pia wameeleza kuwa Damascus inalengwa kutokana na uungaji mkono wake kwa muqawama dhidi ya Magharibi na njama za Wazayuni. Wawakilishi hao pia wametahadharisha pia kuhusu maafa yanayosababishwa na Saudi Arabia nchi ambayo inashiriki katika vita dhidi ya wananchi wa Yemen wasio na hatia.