Walid al Mualim: Marekani inafuatilia malengo ya Israel nchini Syria
Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria amesema kuwa lengo la Marekani ni kudhibiti shughuli zote za Syria kwa maslahi ya Israel.
Walid al Mualim amesema kuwa, Marekani haifuatilii malengo yake pekee nchini Syria bali pia inatekeleza sera za Israel nchini humo.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Syria ameongeza kuwa Washington haitaki Syria iwe kituo kikuu cha mapambano dhidi ya Israel na pia haitaki iwe na uhusiano wa kistratejia na nchi za Iran na Russia. Walid al Mualim ameongeza kuwa, Marekani inafanya kila inachoweza ili kuitumia Syria kama moja ya nyenzo zake za siasa za nje ili kufanikisha maslahi ya Israel.
Mgogoro wa Syria ulianza mwaka 2011 kwa hujuma kubwa ya makundi ya kigaidi yakisaidiwa kwa hali na mali na Saudi Arabia, Marekani na waitifaki wao, lengo likiwa ni kubadili mlingano wa nguvu katika eneo la Mashariki ya Kati kwa maslahi ya utawala haramu wa Israeli.