Nasrallah: Wote wanawajibika kukabiliana na mpango wa 'Muamala wa Karne"
Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon amesema: "Wote wanawajibika kukabiliana na mpango wa Marekani wa "Muamala wa Karne" ambao lengo lake ni kusambaratisha kadhia ya Palestina.
Sayyid Hassan Nasrallah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon ameyasema hayo mjini Beirut Jumamosi alasiri katika hotuba aliyotoa kwa mnasaba wa mwaka wa 19 wa ushindi wa harakati ya muqawama dhidi ya utawala wa Kizayuni na kukombolewa ardhi za Lebanon mwaka 2000. Ameongeza kuwa: "Leo, watu wa Palestina wanakabiliwa na njama kubwa zaidi ya kuwaangamiza na kwa msingi huo, nara na kaulimbiu ya kimsingi ya Siku ya Kimataifa ya Quds mwaka huu, itakayoadhimishwa Ijumaa 31 Mei, ni 'Kukabiliana na Muamala wa Trump."
Kiongozi wa Hizbullah pia amewapongeza maulamaa wa Bahrain kwa msimamo wao wa kimapinduzi na kusisitiza kuwa: "Hatua ya awali ya kutekeleza mpango wa 'Muamala wa Karne, itachukuliwa, Manama, (mji mkuu wa Bahrain). Kuna uwezekano kuwa katika Kongamano la Bahrain, kutachukuliwa hatua za kuwapa Wapalestina makazi ya kudumu nchini Lebanon na nchi zingine, lakini Walebanon wote wamechukua msimamo imara kuhusu kadhia ya Wakimbizi Wapalestina."
Sayyed Hassan Nasrallah ameendelea kusema kuwa: "Adui Mzayuni ameitaja Hizbullah kuwa tishio la kistratijia na kusema uwezo wa kujihami wa Hizbullah ndio chanzo cha kumzuia adui."
Katibu Mkuu wa Hizbullah amesema iwapo harakati ya muqawama na mapambano ya Kiislamu haingekuwpo, leo Rais Trump wa Marekani angekuwa ameukabidhi utawala wa Israel eneo la kusini mwa Lebanon kama alivyofanya kuhusu Miinuko ya Golan ya Syria.
Hassan Nasrallah amesisitiza kuhusu ukombozi wa maeneo ya Lebanon ya Mashamba ya Shebaa na Miinuko ya Kafr Shuma na eneo la al Ghajr yanayokaliwa kwa mabavu na Israel na kuongeza kuwa, hivi sasa Lebanon ina uwezo wa kuizuia Israel kuchimba mafuta na gesi.
Katibu Mkuu wa Hizbullah pia ametoa wito kwa kuondolewa vizingiti ili wakimbizi wa Syria warejee katika nchi yao.