Mufti wa Syria: Bila shaka Wasyria watashinda njama za maadui
Mufti Mkuu wa Syria amesema kuwa, ni suala lisilo na shaka kwamba Wasyria wataibuka washindi dhidi ya njama chafu za maadui, licha ya kuwepo mashinikizo mengi yanayolenga umoja wa kitaifa wa nchi hiyo.
Dakta Ahmad Badreddin Hassoun, Mufti wa Syria ameyasema hayo alipokutana na ujumbe wa Ufaransa unaotembelea Syria na kuongeza kuwa, katika mapambano yao raia wa nchi hiyo dhidi ya magaidi na pia fikra za kufurutu ada zinazotishia usalama wa eneo la Mashariki ya Kati na ulimwengu kwa ujumla, wataibuka washindi dhidi ya njama za maadui. Aidha ameonya juu ya mienendo hasi ya kufurutu ada ya viongozi wa serikali ya Ufaransa na baadhi ya nchi za Magharibi. Katika kikao hicho, ujumbe wa Ufaransa umesisitizia udharura wa kuongezwa juhudi kwa ajili ya kuhitimisha vita vya ndani nchini Syria na pia kurejeshwa usalama na uthabiti ndani ya taifa hilo. Katika hatua nyingine mkuu wa ujumbe unaoiwakilisha serikali ya Syria katika mazungumzo ya Geneva pamoja na wapinzani, amesema kuwa Umoja wa Mataifa kwa mara nyingine umesisitizia umuhimu wa kuendelea mazungumzo hayo bila ya kuhudhuria ujumbe wa Saudia. Bashar Jaafari aliyasema hayo hapo jana na kufuatia maamuzi ya timu ya wapinzani wa serikali wanaoungwa mkono na Saudia, kutishia kususia mazungumzo iwapo timu ya Saudia haitashirikishwa.