OIC yataka kuachiwa huru mateka wa Kipalestina wanaoshikiliwa Israel
Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu (OIC) na Kamati ya Kimataifa ya Msalaba Mwekundu zimetoa wito wa kuachiwa huru mateka wa Kipalestina wanaoshikiliwa katika jela za Israel kutokana na mlipuko wa virusi vya corona.
Taarifa iliyotolewa na Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu imesisitiza udharura wa kuwatetea mateka wote wa Kipalestina walioko katika jela za Israel na kukomeshwa ukiukwaji wa haki zao.
OIC imeashiria hali mbaya ya mateka hao katika jela za utawala haramu wa Israel na kueleza wasiwasi wake kuhusu hali ya baadhi yao waliopatwa na virusi vya corona na kunyimwa matibabu.
Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu imesema kuwa Israel ndiyo inayobeba dhima ya uhai wa maelfu ya Wapalestina wanaoshikiliwa katika jela za utawala huo.
Wakati huo huo Muwaffaq Hamid ambaye ni afisa wa Idara ya Mawasiliano ya Umma ya Jumuiya ya Mateka wa Palestina ametoa wito wa kutumwa timu ya kimataifa ya madaktari katika jela na korokoro za Israel ili kutathmini hali ya kiafya ya mateka hao.
Kabla ya hapo pia kulikuwa kumetolewa ripoti mbalimbali zinazohusiana na mrundikano mkubwa wa mateka na wafungwa wa Kipalestina katika korokoro za utawala haramu wa Israel na hatari kubwa ya maambukizi ya corona katika jela na korokoro hizo.
Hadi sasa mateka wanne wa Kipalestina wameambukizwa corona katika korokoro za Israel kutokana na maambukizi ya COVID-19.