Saudi Arabia, mnunuzi mkuu wa silaha Asia Magharibi
-
Saudia inatumia fedha nyingi kununua silaha na zana za kivita za Magharibi na kuzipachika majina yake kama hili la Al Ashiq
Ripoti mpya iliyotolewa na serikali ya Uingereza inaonesha kuwa, nchi hiyo ilikuwa ya pili kwa kuuza silaha nyingi duniani mwaka uliopita huku mnunuzi mkuu wa silaha za Uingereza katika eneo la Asia Magharibi ukiwa ni utawala wa kiimla wa Saudi Arabia.
Kwa mujibu wa gazeti la Independent, ripoti hiyo ya serikali ya Uingereza inaonesha kuwa, mwaka 2019 mashirika ya silaha ya nchi hiyo yaliuza silaha zenye thamani ya Pound bilioni 11, ikiwa ni asilimia 16 nzima ya silaha zilizouzwa duniani mwaka huo.
Thamani ya silaha za Uingereza zilizouzwa nje ya nchi hiyo kuanzia mwaka 2010 hadi 2019 inakadiriwa kufikia Pound bilioni 86 ambapo asilimia 60 ya silaha hizo zinanunuliwa na nchi za Asia Magharibi. Sehemu kubwa ya silaha za Uingereza zilizouzwa nje ya nchi katika kipindi hicho ni za anga na anga za mbali pamoja na aina mbalimbali za rada, makombora na ndege za kivita. Wanunuzi wakuu wa silaha hizo ni Saudi Arabia, Uturuki, Oman, Marekani na Qatar.
Andrew Smith, Msemaji wa Kampeni ya Kupiga Vita Mauzo ya Silaha amesema: Madalali wa silaha wanafurahishwa na jambo hilo wakati idadi kubwa kama hiyo ya silaha inabidi iwe ni aibu na fedheha kwa wauzaji na wanunuzi wake.
Amesema, Waziri Mkuu wa Uingereza, Boris Johnson na wenzake muda wote utawasikia wanazungumzi aUingereza ya Kimataifa na umuhimu wa kulindwa haki za binadamu na uhuru wa kusema, lakini wakati huo huo wanaunga mkono kikamilifu ukandamizaji na ukatili unaofanyika katika kona zote za dunia kwa kutumia silaha za Uingereza.
Taarifa zinasema kuwa, Uingereza inazipa silaha zaidi ya nchi 10 zinazovunja haki za binadamu hasa Saudi Arabia, kinyume kabisa na sheria hata za ndani ya Uingereza kwenyewe.