Walowezi wa Kizayuni wawashambulia Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i77182-walowezi_wa_kizayuni_wawashambulia_wapalestina_katika_ukingo_wa_magharibi
Makumi ya walowezi wa Kizayuni wamefanya hujuma na mashambulio dhidi ya nyumba za Wapalestina kusini mwa mji wa Nablos ulioko kaskazini mwa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu.
(last modified 2026-02-05T09:20:29+00:00 )
Nov 22, 2021 04:41 UTC
  • Walowezi wa Kizayuni wawashambulia Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi

Makumi ya walowezi wa Kizayuni wamefanya hujuma na mashambulio dhidi ya nyumba za Wapalestina kusini mwa mji wa Nablos ulioko kaskazini mwa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu.

Ripoti zinasema, hujuma na mashambulio hayo ya walowezi wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina huko katika mji wa Nablos yamefanyika usiku wa kuamkia leo.

Inaelezwa kuwa, mbali na hujuma hiyo, Wazayuni hao wameharibu magari kadhaa ya Wapalestina katika eneo hilo.

Katika mji wa Quds pia, Wazayuni wakiungwa mkono na kupata himaya ya jeshi la utawala haramu wa Israel wamewashambulia Wapalestina na kuwapiga.

Hayo yanaripotiwa katika hali ambayo, hivi karibuni, mabuldoza ya utawala haramu wa Kizayuni wa Israel yalivamia maeneo ya kaskazini mwa mji wa Quds na kuharibu mali na miliki za Wapalestina katika maeneo hayo.

Buldoza la utawala haramu wa Israel likibomoa nyumba za Wapalestina chini ya usimamizi wa wanajeshi wa Kizayuni

 

Wanajeshi wa Israel wakiongozwa na mabuldoza walivamia kitongoji kimoja jirani na kivuko cha Qalandiya kaskazini mwa Quds inayokaliwa kwa mabavu na kuharibu mali na miliki kadhaa za Wapalestina.

Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa (OCHA) imesema katika ripoti yake kwamba, vitendo vya ukandamizaji vinavyofanywa na Israel vimeshadidi mno tangu kuanza mwaka huu wa 2021.

Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa, mwaka uliopita wa 2020 utawala wa Kizayuni wa Israel ulibomoa nyumba karibu 689 katika Ukingo wa Magharibi na Quds tukufu na kulazimisha mamia ya familia za Wapalestina kuwa wakimbizi.