Katibu Mkuu wa Jihadul-Islami: Damu ya Mashahidi itailetea ushindi Palestina
Feb 25, 2023 03:39 UTC
Katibu Mkuu wa Harakati ya Jihadul-Islami ya Palestina amepongeza mchango wa kijihadi wa Mashahidi wa ardhi hiyo katika kukabiliana na adui Mzayuni na akasema, damu za Mashahidi hao ndizo zitakazoiletea ushindi Palestina.
Kwa mujibu wa ripoti ya tovuti ya habari ya Palestina Al-Yaum Ziyad Al-Nakhlah, Katibu Mkuu wa Harakati ya Jihadul-Islami ya Palestina, amesema hayo katika mazungumzo aliyofanya kwa njia ya simu na familia za Mashahidi wa Nablus na Jenin, ambapo sambamba na kuzifariji familia za Mashahidi hao, ametoa salamu zake za rambirambi kwa kuuawa shahidi Wapalestina hao na kusisitiza kuwa damu ya Mashahidi ambayo imewasha mwenge wa mapinduzi matunda yake yatapatikana kwa ushindi wa Palestina.

Al-Nakhlah ameongeza kuwa, Harakati ya Jihadul-Islami ya Palestina inasimama bega kwa bega na familia za Mashahidi na haitaacha kutekeleza jukumu lake la kudumu katika utiifu na uaminifu kwa Waplestina waliojitoa mhanga na kuendelea kuwafuata mashahidi hao hadi utakapotekelezwa usia wao wa kurejeshwa uhuru na haki kwa taifa la Palestina na Umma wa Kiislamu.
Inafaa kuashiria kuwa, Wapalestina 11 wameuawa shahidi na wengine wasiopungua 100 wamejeruhiwa katika jinai iliyofanywa hivi karibuni na askari katili wa utawala haramu wa wa Kizayuni wa Israel katika mji wa Nablus Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.../
Tags