Msikiti mwingine washambuliwa na watu wenye chuki Canada
Polisi ya Canada imetangaza habari ya kushambuliwa msikiti na watu wenye chuki dhidi ya dini ya Kiislamu katika mji wa Montreal nchini humo.
Taarifa iliyotolewa na polisi ya Canada imesema kuwa, watu wasiojulikana waliushambulia jana msikiti wa mji wa Montreal, mashariki mwa nchi hiyo na kwamba shambulio hilo limepelekea kuvunjika madirisha ya msikiti huo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, tayari polisi wameanzisha uchunguzi wenye lengo la kuwabaini wahusika wa hujuma hiyo. Shambulizi hilo limetokea ikiwa ni siku nne zimepita tangu kuliipojiri shambulizi la kigaidi katika mji wa Quebec nchini humo ambapo watu sita waliokuwa wakisali msikitini hapo waliuawa.
Kufuatia shambulizi hilo, Justin Trudeau, Waziri Mkuu wa Canada alitoa mkono wa pole kwa Waislamu wa nchi hiyo kama ambavyo alitangaza kuungana nao katika msiba huo. Aidha Trudeau alishiriki pia mazishi ya Waislamu watatu wa hujuma hiyo yaliyofanyika siku ya Alkhamisi iliyopita. Uchunguzi wa awali uliofanywa na polisi ya Canada unaonyesha kwamba, mwanafunzi wa chuo kikuu aliyetekeleza mauaji dhidi ya Waislamu wa mjini Quebec ni mtu mwenye misimamo ya mrengo wa kulia na mfuasi sugu wa Donald Trump, rais mpya wa Marekani.
Mashambulizi na hujuma dhidi ya Waislamu katika maeneo mbalimbali duniani vimeshadidi tangu alipoingia madarakani rais huyo mwenye chuki dhidi ya Waislamu.