IAEA: Hatujapokea taarifa yoyote kutoka Marekani kuhusu JCPOA
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA), Yukia Amano, amesema taasisi hiyo haijapokea taarifa wala kufanya mawasiliano yoyote na Marekani kuhusu msimamo wa Washington juu ya makubaliano ya nyuklia ya Iran.
Katika mahojiano na shirika la habari la AP, Amano amesema huko nyuma aliwasiliana sana na maafisa wa Washington kuhusu makubaliano ya nyuklia ya Iran, lakini tangu serikali mpya ya Rais Donald Trump iingie madarakani, hajapokea simu yoyote kutoka Marekani juu ya kadhia hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki amesema anatumai kuwa wakuu wa Washington watalipa suala hilo uzito na kuwasiliana naye katika siku chache zijazo.
IAEA imetangaza mara kadhaa kuwa Iran imetekeleza majjukumu yake katika mapatano hayo ya nyuklia ambayo yalitiwa sainai Julai mwaka 2015 na kuanza kutekelezwa Januari mwaka jana.
Hata hivyo, Trump aliwahi kusema wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais kuwa, mapatano ya nyuklia ya Iran ni 'maafa na ni makubaliano mabaya zaidi duniani' na kuahidi kuyachana katika siku yake ya kwanza atakapoingia kwenye Ikulu ya White House.