Marekani yawataka Wapalestina wasisogelee maeneo yanayokaliwa kwa mabavu
Mjumbe Maalumu wa Marekani katika Masuala ya Mashariki ya Kati amewataka wafanya maaadamano wa Palestina wasisogelee mpaka wa Ukanda wa Ghaza na ardhi zinazokaliwa kwa mabavu na Israel.
Jason Greenblatt amesema kuwa Marekani inawataka wafanya maandamano wa Kipalestina kuandamana kwa amani na kwamba hawapasi kusogea karibu na mpaka huo kivyovyote vile.
Katika upande mwingine Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres ameutaka utawala wa Kizayuni wa Israel ujiepushe kuutumia mabavu ili kuzuia uwezekano wowote wa kutokea maafa. Guterres amesema kuwa raia wana haki ya kuandamana kwa amani.
Awali Waziri wa Vita wa utawala wa Kizayuni wa Israel, Avigdor Lieberman alitoa tahadhari kutokana na kukaribia kufanyika maandamano ya leo ya wakazi wa Palestina wa Ukanda wa Ghaza na kusema kuwa jibu litakalotolewa kwa hatua ya kichochezi ya Wapalestina litakuwa sawa na lile la Ijumaa iliyopita.
Hadi kufikia sasa zaidi ya Wapalestina 20 wameuliwa shahidi na wengine zaidi ya 1900 kujeruhiwa tangu Ijumaa iliyopita wakati wa maandamano ya wananchi wa Palestina yaliyofanyika chini ya anwani ya "Haki ya Kurejea". Maandamano hayo yalifanyika tarehe 30 mwezi uliopita kwa mnasaba wa kuadhimisha Siku ya Ardhi na yangali yanaendelea.