Wanawake Waislamu Denmark wapigwa marufuku kuvaa niqabu
Serikali ya Denmark imepiga marufuku vazi la burqa au niqabu linalovaliwa na baadhi ya wanawake wa Kiislamu.
Bunge la Denmark jana Alkhamisi lilipasisha kwa wingi wa kura muswada wa sheria inayowapiga marufuku wanawake Waislamu kuvaa vazi hilo katika maeneo ya umma.
Kwa mujibu wa sheria hiyo, mwanamke Muislamu atakayekamatwa mara ya kwanza kwa kuvaa niqabu katika maeneo ya umma atatozwa faini ya Crown 1000 sarafu ya nchi hiyo, sawa na dola 160 za Marekani, na iwapo atakiuka sheria hiyo hadi mara ya nne, atatozwa faini ya Crown 10,000.
Sheria hiyo inatazamiwa kuanza kutekelezwa Agosti Mosi mwaka huu, huo ukiwa ni muendelezo wa kuwabana zaidi Waislamu na dini yao tukufu.
Mapema mwaka huu, Bunge la Denmark lilifuta sheria iliyopitishwa miaka 334 iliyopita inayopiga marufuku kuzivunjia heshima dini hadharani ikiwemo kuchoma moto Vitabu vitakatifu.
Nchi kadhaa za magharibi kama vile Austria, Bulgaria, Canada, Ubelgiji na Ufaransa zimepiga marufuku vazi hilo kuvaliwa katika maeneo ya umma.