UN: Kiwango cha njaa duniani kimeongezeka kwa mwaka wa tatu mtawalia
Umoja wa Mataifa umetahadharisha kuwa kiwango cha njaa duniani mwaka jana kiliongezeka kwa mwaka wa tatu mtawalia kutokana na mizozo ya kivita na mabadiliko ya tabia nchi.
Ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya usalama wa chakula na lishe duniani mwaka huu wa 2018 inaonyesha kuwa kiwango cha njaa kinaonekana kuongezeka katika maeneo mengi ya Afrika na Amerika ya Latini. Ripoti ya Umoja wa Mataifa inaonyesha kuwa kati ya watu milioni 821, mtu mmoja kati ya watu tisa alisalia na njaa katika mwaka uliopita wa 2017. Wakati huo huo watu wazima milioni 672 wana unene wa kupindukia kulinganisha na watu milioni 600 waliokuwa na hali hiyo mwaka 2014.
Ripoti hii ya Umoja wa Mataifa imeongeza kuwa iwapo jitihada zaidi hazitachukuliwa kuna hatari ya kutofanikishwa malengo ya maendeleo ya milenia (SGD's) ya kukomesha njaa ifikapo mwaka 2030. Mwaka jana karibu watu milioni 124 katika nchi 51 duniani walikabiliwa na mgogoro wa njaa uliosababishwa na mizozo ya kivita na majanga ya mabadiliko ya tabia nchi.
