Umoja wa Mataifa: Myanmar si mahali salama kwa Waislamu Warohingya
Umoja wa Mataifa umeeleza katika ripoti yake mpya kuhusu Myanmar kuwa serikali ya nchi hiyo haijatayarisha mazingira yoyote kuwawezesha Waislamu Warohingya kurejea kwenye maisha yao ya kawaida.
Ripoti hiyo iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR na Mpango wa Ujenzi wa umoja huo imesisitiza kuwa Waislamu Warohingya wangali wanaishi kwa hofu na kutokuwa na imani yoyote kuhusu usalama wao wakiwa hawana hata ruhusa ya kutembea kwa uhuru katika eneo wanaloishi la mkoa wa Rakhine.
Msemaji wa UNHCR amesema, Waislamu hao wanashindwa kukidhi mahitaji yao ya kila siku kutokana na kutokuwepo usalama na vizuizi vya kutembea walivyowekewa.
Andrej Mahecic ameashiria safari aliyofanya yeye mwenyewe kutembelea maeneo ya Waislamu katika mkoa wa Rakhine nchini Myanmar na kueleza kwamba: Watu wa eneo hilo walimweleza kuwa huduma za afya na elimu hazipatikani kutokana na vizuizi walivyowekewa Waislamu wa jamii ya Rohingya.
Hii ni katika hali ambayo mnamo mwezi Juni mwaka huu serikali ya Myanmar iliyaahidi mashirika ya Umoja wa Mataifa kwamba itaandaa mazingira ya kudhamini urejeaji wa hiyari, wa salama na endelevu kwa Waislamu Warohingya walioko Bangladesh na kuwapatia tena makazi mapya katika mkoa wa Rakhine.
Kwa mujibu wa Mahecic tathmini zilizofanywa zinaonyesha kuwa serikali ya Myanmar haijachukua hatua hata moja kati ya hizo hadi sasa.
Mwaka uliopita wa 2017, Waislamu wapatao laki saba wa jamii ya Rohingya walilazimika kukimbilia Bangladesh kutokana na mauaji, ukatili na ubakaji waliokuwa wakifanyiwa na jeshi la Myanmar na mabudha wenye misimamo ya kufurutu mpaka.../