Joe Biden aendeleza uhasama wa Marekani dhidi ya Iran
-
Joe Biden
Rais Joe Biden wa Marekani amedai katika mahojiano yake na gazeti la Washington Post, kuwa Washington itaendeleza mashinikizo ya kidiplomasia na kiuchumi hadi Iran itakaporejea kwenye makubaliano ya nyuklia ya JCPOA.
Katika matamshi hayo yaliyotolewa kabla ya kuanza safari yake eneo la Asia Magharibi wiki ijayo, Rais wa Marekani ameihujumu Iran kuhusiana na mazungumzo ya nyuklia akidai kuwa Tehran imetengwa hadi irejee kwenye makubaliano hayo.
Joe Biden pia amedai kwamba, "utawala wake utaendelea kuzidisha mashinikizo hadi Iran irejee kwenye makubaliano ya nyuklia na kutekeleza majukumu yake."
Itakumbukwa kuwa, mwezi Mei mwaka 2018 Washington ilijiondoa kwa upande mmoja na kinyume cha sheria katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA wakati wa uongozi wa Donald Trump, na tangu wakati huo, sambamba na kurejesha vikwazo vya nyuklia, pia imeiweka Jamhuri ya Kiislamu vikwazo vikubwa zaidi. Biden aliwaahidi Wamarekani kwamba atairejesha nchi hiyo kwenye makubaliano ya nyuklia ya JCPOA; hata hivyo, hadi sasa hakuna hatua yoyote ya kivitendo iliyochukuliwa na serikali ya Washington katika uwanja huo.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imekuwa ikisisitiza kwamba itatekeleza kikamilifu makubaliano ya nyuklia ya JCPOA iwapo vikwazo vyote ilivyowekewa na Marekani vitafutiliwa mbali na mapatano ya JCPOA yatekelezwe na pande nyingine husika kwa namna itakayoiruhusu Iran kufaidika na maslahi yake chini ya mkataba huo wa kimataifa.