Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Shanghai afanya mazungumzo na Rais wa Iran
Zhang Ming Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai leo Alhamisi amekutana na kufanya mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika mji wa Samarkand.
Rais Sayyid Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran jana Jumatano alielekea Uzbekistan akiambatana na ujumbe wa ngazi ya juu wa kisiasa na kiuchumi kufuatia mwaliko rasmi wa Rais Shavkat Mirziyoyev wa Uzbekistan. Rais wa Iran ameelekea Uzbekistan kwa ziara rasmi ya mazungumzo ya pande mbili na kwa ajili pia ya kushiriki katika Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai.
Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai iliundwa huko Shanghai tarehe 15 Juni mwaka 2001 na nchi za Kazakhstan, China, Kyrgyzstan, Russia, Tajikistan na Uzbekistan. Aidha India, Kazakhstan,China, Kyrgyzstan, Pakistan, Russia, Tajikistan na Uzbekistan ni nchi nane zilizoko katika jumuiya hiyo ya kiuchumi ya kikanda ya Shanghai.
Wakati huo huo, Iran imepongeza kusainiwa hati ya utekelezaji ya kujiunga na Jumuiya ya Ushirikiano ya Shanghai (SCO), na hivyo kuingia katika marhala mpya ya maingiliano na taasisi hiyo. Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Hossein Amir-Abdollahian alitangaza kusainiwa kwa waraka huo kupitia taarifa aliyotuma katika ukurasa wake wa tweeter jana Jumatano.