Aug 07, 2018 02:18 UTC
  • Jumanne, Agosti 7, 2018

Leo ni Jumanne tarehe 24 Mfunguo Pili Dhulqaada 1439 Hijria sawa na Agosti 07 mwaka 2018 Milaadia.

Siku kama ya leo miaka 1239 iliyopita kwa mujibu wa kalenda ya Hijria, Imam Ridha (a.s) aliondoka mjini Madina na kuanza safari yake ya kuelekea Marw kaskazini mashariki mwa Iran ya kale. Imam Ridha alifanya safari hiyo kwa lazima na mashinikizo ya Maamun Khalifa wa Saba wa utawala wa Bani Abbas. Lengo la Maamun kutaka Imam Ridha apelekwe Marw lilikuwa kumfanya awe karibu na hivyo kudhibiti nyendo zake. Japokuwa kidhahiri Maamun alimfanya Imam kuwa mrithi wa kiti, cheo ambacho Imam Ridha alikikubali kwa kulazimishwa, lakini uhakika wa mambo ni kuwa alitaka kuimarisha misingi ya utawala wake. Imam Ridha aliendelea kuutambua utawala wa Maamun kwamba, si halali na alikuwa akifichua uovu na dhulma za utawala huo. Hatimaye Maamun alishindwa kuvumilia shakhsia ya kielimu na kimaanawi ya Imam pamoja na ushawishi wake kwa watu, hivyo akaamua kumpa sumu na kumuua shahidi. 

Njia ya Imam kuelekea Marw

Siku kama ya leo miaka 36 iliyopita mwafaka na tarehe 7 Agosti 1982, yalitiwa saini makubalino ya kuondoka vikosi vya Harakati ya Ukombozi ya Palestina (PLO) mjini Beirut Lebanon kati ya Marekani, Lebanon na PLO. Makubaliano hayo yalitiwa saini kufuatia shambulio kubwa lililofanywa na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel nchini Lebanon mwezi Juni 1982 kwa shabaha ya kuwafukuza wapiganaji wa PLO nchini Lebanon. Ijapokuwa kuondoka wanamgambo wa PLO nchini Lebanon kulitoa pigo kubwa kwa harakati hiyo, lakini miaka ya baadaye Wazayuni maghasibu walikabiliwa na kipigo kikali kutoka kwa wanamapambano wa harakati ya Hizbullah ya Lebanon, na kulazimika kuondoka kwa madhila katika ardhi ya nchi hiyo mwaka 2000.

Yasir Arafat

Siku kama ya leo miaka 58 iliyopita sawa na Agosti 7 1960 nchi ya Ivory Coast ilifanikiwa kujipatia uhuru kutoka kwa mkoloni Mfaransa. Wareno waliidhibiti nchi hiyo iliyoko magharibi mwa Afrika katika karne ya 16, lakini ulipofika mwaka 1891 Ufaransa iliidhibiti nchi hiyo, licha ya upinzani mkubwa wa wananchi wa Ivory Coast. Hatimaye ulipofika mwaka 1960, Ivory Coast ikiwa pamoja na nchi nyingine kadhaa za Kiafrika zilizokoloniwa na Mfaransa zilijipatia uhuru wao.

Bendera ya Ivory Coast

Na Siku kama ya leo miaka 10 iliyopita vikosi vya jeshi la Georgia vikisaidiwa na serikali ya Marekani vililishambulia eneo linalopigania kujitenga la Ossetia ya Kusini huko kaskazini mwa nchi hiyo. Mamia ya raia wasio na hatia wala ulinzi waliuawa na kujeruhiwa kwenye mashambulio hayo. Siku moja baadaye, wanajeshi wa Russia waliingilia kati na kuamua kuwaunga mkono wapiganaji wanaopigania kujitenga wa Ossetia ya Kusini na kulilazimisha jeshi la Georgia kurudi nyuma. Vikosi vya jeshi la Russia vilifanikiwa kuiteka bandari muhimu ya Patumi na kusonga mbele karibu na Tiblis mji mkuu wa nchi hiyo. Jeshi la Russia liliondoka huko Georgia Agosti 12 kwa upatanishi wa Rais wa Ufaransa, na Moscow ikayatambua rasmi kuwa huru maeneo mawili yaliyokuwa yakipigania kujitenga yaani Ossetia ya Kusini na Abkhazia.

Tags