Ripoti ya UN: RSF inashambulia na kuua raia Darfur, Sudan kwa msingi wa ukabila
Ripoti mpya ya wataalamu wa Umoja wa Mataifa imesema, Vikosi vya Usaidizi wa Haraka RSF pamoja na wanamgambo vinaoshirikiana nao wanaopigania kutwaa madaraka nchini Sudan wamefanya mauaji ya kikabila na ubakaji wakati wa udhibiti wa eneo kubwa la Darfur magharibi mwa nchi hiyo, na kwamba vitendo hivyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu.
Mapigano hayo yameenea katika maeneo mengine ya nchi, lakini yamechukua sura tofauti katika jimbo la Darfur, ambako wanamgambo wa RSF wamefanya mashambulizi ya kikatili dhidi ya raia Waafrika, hasa wa kabila la Masalit.
Miongo miwili iliyopita, Darfur ilijulikana kwa mauaji ya kimbari na uhalifu wa kivita, hasa uliofanywa na wanamgambo maaarufu wa Janjaweed dhidi ya watu wanaotambuliwa kama Waafrika wa Kati au Mashariki.
Inavyoonekana, hali ileile ya wakati huo imerejea tena, kiasi kwamba Mwendesha Mashtaka wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC Karim Khan alitangaza mwishoni mwa Januari kwamba, kuna sababu za kuamini kuwa pande zote mbili zinazopigana nchini Sudan zinafanya uhalifu wa kivita, uhalifu dhidi ya binadamu au mauaji ya kimbari huko Darfur.
Mzozo unaoendelea nchini Sudan umesababisha hali mbaya sana ya kibinadamu na kupelekea watu wapatao milioni sita na laki nane kuyahama makazi yao, milioni tano na laki nne wakibaki bila makazi ndani ya nchi hiyo na milioni moja na laki nne ambao wamekimbilia nchi nyingine, wakiwemo laki tano na nusu waliotafuta hifadhi katika nchi jirani ya Chad.../