Kura zaanza kuhesabiwa Uganda, mitandao ya kijamii yafungwa
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i1495-kura_zaanza_kuhesabiwa_uganda_mitandao_ya_kijamii_yafungwa
Uchaguzi wa rais na bunge nchini Uganda ambao ulianza saa moja asubuhi leo kwa saa za nchi hiyo katika vituo vingi vya kupiga kura umemalizika saa moja jioni bila kuripotiwa visa vikubwa vya uhalifu na uchakachuaji.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Feb 18, 2016 13:12 UTC
  • Kura zaanza kuhesabiwa Uganda, mitandao ya kijamii yafungwa

Uchaguzi wa rais na bunge nchini Uganda ambao ulianza saa moja asubuhi leo kwa saa za nchi hiyo katika vituo vingi vya kupiga kura umemalizika saa moja jioni bila kuripotiwa visa vikubwa vya uhalifu na uchakachuaji.

Mwenyeti wa Tume ya Uchaguzi Uganda, Badru Kiggundu aliongeza muda wa kupiga kura kutoka saa kumi jioni ambao vituo vyote vilitazamiwa viwe vimefungwa hadi saa moja jioni katika vituo ambavyo vilipokea masanduku na makaratasi ya kupigia kura kwa kuchelewa. Hadi tunaenda mitamboni zoezi la kuhesabu kura lilikuwa linaendelea katika vituo vingi. Timu ya waangalizi wa Umoja wa Ulaya EU imesema kuwa asilimia 41 ya vituo vilipokea vifaa vya kupigia kura kwa wakati na kwamba mpaka sasa zoezi hilo la kidemokrasia linaendelea vizuri. Wakati huo huo, Rais Yoweri Museveni ametetea hatua ya kufungwa kwa mitandao ya kijamii kama vile facebook, twitter na Whatsapp akisisitiza kuwa imetokana na sababu za kiusalama. Rais Museveni ambaye ameongoza nchi hiyo kwa miongo mitatu sasa amesema kuwa wamechukua hatua hiyo baada ya kuona baadhi ya wananchi wanatumia mitandao ya kijamii kueneza woga na propaganda. Mapema leo, Mkuu wa ujumbe wa AU, Sophia Okofor pia amewataka raia wa Uganda kudumisha amani na kuwa watulivu baada ya uchaguzi. Wapigakura waliojiandikisha ni takriban milioni 15.3 na kuna vituo 28, 010 kote nchini Uganda. Wagombea urais ni wanane na kwa upande wa bunge, viti vinavyowaniwa ni 290. Nafasi ya Urais imewavutia wagombea 8 akiwemo Rais Yoweri Museveni na Waziri Mkuu wa zamani, Amama Mbabazi pamoja na mpinzani wa muda mrefu wa serikali, Dk. Kizza Besigye.