Siku ya Hijabu ya Waridi yaadhimishwa nchini Tanzania
Sherehe ya kuadhimisha Siku ya Hijabu ya Waridi imefanyika leo mjini Dar es Salaam, Tanzania kwa ushirikiano wa ofisi ya Mwambata wa Utamaduni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Mwenyekiti Taifa wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislam nchini Tanzania (JUWAKITA), Shamim Khan ambaye amehutubia sherehe hiyo amesema kuwa vazi la mwanamke wa Kiislamu la hijabu ni kito chenye thamani kubwa kwa wanawake na ngao inayowalinda wanawake Waislamu.
Shamim Khan ameongeza kuwa, hijabu haiishi katika vazi tu bali ni mtindo wa maisha na kielelezo cha utakasifu na heshima ya wanawake. Amesema wakati mwanamke anapolinda na kuheshimu vazi lake la hijabu hupata kinga mbele ya matatizo mengi.
Mwenyekiti JUWAKITA amesema kuwa, utamaduni wa Magharibi hauwezi kumuokoa mwanamke wa Kiislamu bali unamharibu na kuuangamiza na kueneza utovu wa haya na heshima katika jamii.
Sherehe hiyo ya Siku ya Hijabu ya Waridi nchini Tanzania imefanyika kwa ushirikiano wa Jumuiya ya Wanawake wa Kiislam Tanzania (JUWAKITA), ofisi ya Mwambata wa Utamaduni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mjini Dar es Salaam na taasisi nyingine za Tanzania. Sherehe hiyo hufanyika kila mwaka kwa shabaha ya kuhimiza umuhimu wa vazi la hijabu la mwanamke wa Kiislamu.