Hali ya kibinadamu Jamhuri ya Afrika ya Kati inatia wasiwasi
Mratibu wa Masuala ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati amesema kuwa hali ya kibinadamu nchini humo inatia wasiwasi.
Michel Yao Mratibu wa Masuala ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati amesema kuwa hali ya kibinadamu na kiusalama katika maeneo mengi ya nchi hiyo inatia wasiwasi. Yao amebainisha kuwa kuongezeka mivutano na mapigano kati ya makundi hasimu yenye silaha huko Jamhuri ya Afrika ya Kati kumesababisha maelfu ya raia kuwa wakimbizi na kuongezeka pakubwa mahitaji ya kibinadamu.
Mratibu wa Masuala ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati amesema kuwa mji wa Bambari unaopatikana katikati mwa nchi hiyo umepokea wakimbizi wapya zaidi ya 26,000 tangu mwezi Januari hadi mwezi huu wa Machi; na katika maeneo ya kaskazini na magharibi mwa nchi kuna wakimbizi wengine zaidi ya elfu 30. Michel Yao ameyatahadharisha makundi yenye silaha kuhusu taathira hasi za hujuma dhidi ya raia na kuitolea mwito jamii ya kimataifa kuisaidia zaidi serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.