Jul 20, 2017 04:06 UTC
  • Jeshi la Congo latakiwa kukomesha mapigano mashariki mwa nchi

Viongozi wa eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo wamelitaka jeshi la nchi hiyo kukomesha mapigano yanayoendelea katika eneo hilo.

Viongozi wa eneo la Lubero katika mkoa wa Kivu Kaskazini wametangaza kuwa, mapigano hayo makali yalianza Jumatatu iliyopita katika eneo la Walikale kati ya waasi wa Mai Mai na kundi la NDC na wamelitaka jeshi kuingilia haraka na kukomesha mapigano hayo haraka iwezekanavyo.

Viongozi wa eneo la Lubero wamesema kuwa, idadi kubwa ya wanavijiji wamelazimika kukimbia makazi yao kutokana na mapigano hayo. Wamesisitiza kuwa, kuna udharura wa jeshi la serikali kuchukua hatua za haraka za kusitisha mapigano hayo na kuokoa maisha ya raia.

Jeshi la Congo latakiwa kuokoa maisha ya raia, Walekale

Msemaji wa Operesheni ya Jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo mashariki mwa nchi hiyo maarufu kwa jina la Sokola -1, Jules Ngongo amesema jeshi linajitayarisha kwa ajili ya kurejesha amani katika eneo hilo.

Ripoti zinasema kuwa, watu wasiopungua 13 wameuawa hadi sasa katika mapigano yanayoendelea katika eneo la Walikale. 

Maeneo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo yameendelea kusumbuliwa na mapigano makali kati ya makundi hasimu na vilevile kati ya jeshi la serikali na baadhi ya makundi ya waasi.   

Tags