Basi lililokuwa likielekea A/Kusini laripuka na kuua abiria 43 Zimbabwe
Watu wasiopungua 43 wamethibitishwa kupoteza maisha baada ya basi la abiria kuripuka na kushika moto usiku wa kuamkia leo nchini Zimbabwe.
Charity Charamba, msemaji wa Polisi ya Zimbabwe amesema leo Ijumaa kuwa, basi hilo lilikuwa likielekea katika nchi jirani ya Afrika Kusini na kwamba makumi ya abiria wengine wamejeruhiwa kwenye ajali hiyo.
Duru za habari zinaarifu kuwa, yumkini mtungi wa gesi wa mmoja wa abiria uliripuka ndiposa basi hilo likashika moto na kuungua hadi likabakia majivu.
Mashuhuda wanasema ajali hiyo ilitokea katika barabara kuu ya Beitbridge kuelekea Bulawayo.

Haya yanajiri wiki moja baada ya watu wengine 47 kufariki dunia katika ajali nyingine iliyohusisha mabasi mawili ya abiria. Mabasi hayo yaligongana ana kwa ana katika barabara iliyoko katikati ya mji mkuu Harare na mji wa Rusape.
Aidha Juni mwaka jana, watu wengine 43 waliaga dunia katika ajali nyingine iliyohusisha basi la abiria kaskazini mwa nchi, karibu na mpaka wa nchi hiyo na Zambia.