Watunisia waendeleza maandamano dhidi ya serikali
Baada ya kijana mmoja kufariki dunia, raia wa Tunisia wamemiminika barabarani na kuandamana dhidi ya serikali ya nchi hiyo.
Katika maandamano hayo yaliyoanza Ijumaa usiku katika eneo la Al-Awamia, katikati ya mji wa Tunis, mji mkuu wa nchi hiyo na ambalo ni eneo alikozaliwa kijana huyo, waandamanaji wamefunga njia kuu huku polisi wakiwatawanya kwa kutumia mabomu ya kutoa machozi. Ijumaa usiku kuliibuka vurugu kubwa kati ya waandamanaji na polisi katika eneo la Braque al-Sahel, kusini mashariki mwa mji wa Tunis ambapo kijana mmoja alipoteza maisha. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kabla ya kijana huyo kutiwa mbaroni na kuhamishiwa kituo cha polisi, alipigana na kijana mwingine na ikawa sababu ya kifo chake, ingawa hadi sasa haijafahamika iwapo kijana huyo alifariki dunia ndani ya kituo cha polisi au kabla ya kufikishwa kituoni hapo.
Kuhusu suala hilo, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Tunisia imetoa taarifa ikisema kuwa, kijana huyo alifariki dunia kutokana na mshtuko aliopata ambapo alipofikishwa polisi tayari alikuwa ameenda koma, huku juuhudi za maafisa wa polisi kwa ajili ya kuokoa maisha yake zikifeli. Kwa sasa Tunisia inaendelea kushuhudia wimbi la malalamiko ya wananchi. Mwezi Disemba mwaka jana pia kijana mmoja alijichoma moto katika kulalamikia hali mbaya ya kiuchumi na kijamii, katika hali ambayo maandamano ya mwaka 2011 pia yalichochewa na kitendo cha kijana Mohamed Bouazizi kujichoma moto.