Polisi ya Uganda 'yamkamata tena' Bobi Wine na timu yake ya kampeni
Kwa mara nyingine tena, jeshi la polisi la Uganda limeripotiwa kumtia mbaroni Bobi Wine, kiongozi machachari wa upinzani nchini humo ambaye pia ni mgombea wa urais katika uchaguzi wa mapema mwakani.
Wine ametangaza habari ya kukamatwa kwake katika ujumbe aliotuma leo Jumatano kwenye ukurasa wake rasmi wa mtandao wa kijamii wa Twitter bila kutoa maelezo ya kina.
Inasemekana kuwa, mwanasiasa huyo chipukizi amekamatwa katika eneo la Kalangala la katikati mwa nchi, akiwa pamoja na wakuu wa timu ya kampeni zake za urais.
Haya yanajiri masaa machache baada ya Wine ambaye kwa sasa ni Mbunge wa eneo la Kyadondo kusisitiza kuwa ataendeleza kampeni zake za urais katika maeneo yote ya nchi licha ya Tume ya Uchaguzi ya nchi hiyo kutangaza kusitisha kampeni hizo katika baadhi ya maeneo kwa kisingizio cha kuzuia kuenea zaidi virusi vya Corona.
Miji ambayo mikutano ya kampeni imesitishwa kuanzia Jumamosi iliyopita mbali na mji mkuu Kampala ni Mbarara, Kabarole, Luwero, Kasese, Masaka, Wakiso, Jinja, Kalungu, Kazo na Tororo.
Tume ya Uchaguzi Uganda (EC) imetangaza tarehe 14 Januari mwaka ujao 2021 kuwa siku ya kufanyika uchaguzi mkuu, ambapo Rais Yoweri Museveni anayeiongoza nchi hiyo kwa zaidi ya miaka 30 sasa anatazamiwa kuchuana vikali na Bobi Wine wa chama cha upinzani cha NUP katika uchaguzi wa urais.