Museveni: Uganda inaridishwa na uhusiano wake wa kiulinzi na Russia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i95560-museveni_uganda_inaridishwa_na_uhusiano_wake_wa_kiulinzi_na_russia
Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda amepongeza ushirikiano mzuri wa kiulinzi na kijeshi wa Kampala na Moscow na kusisitiza kuwa, Uganda na Russia zimekuwa na mahusiano ya kuridhisha tangu enzi za Sovieti.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Mar 26, 2023 22:42 UTC
  • Museveni: Uganda inaridishwa na uhusiano wake wa kiulinzi na Russia

Rais Yoweri Kaguta Museveni wa Uganda amepongeza ushirikiano mzuri wa kiulinzi na kijeshi wa Kampala na Moscow na kusisitiza kuwa, Uganda na Russia zimekuwa na mahusiano ya kuridhisha tangu enzi za Sovieti.

Museveni amesema hayo katika mahojiano na shirika la habari la TASS na kueleza kuwa, "Leo hii, tunaridhishwa na ushirikiano wetu na Shirikisho la Russia. Tunashirikiana katika uga wa ulinzi, na tunanunua silaha na teknojia ya hali ya juu."

Kadhalika Rais wa Uganda amethibitisha kuwa atashiriki mkutano ujao wa Russia na Uganda unaotazamiwa kufanyika mwezi Julai mwaka huu mjini St.Petersburg.

Museveni amebainisha kuwa, licha ya uhusiano wa Uganda na Russia kuyumba kidogo wakati wa kuanguka kwa Umoja wa Sovieti, lakini nchi mbili hizo daima zimekuwa na ukuruba.

Rais Vladimir Putin wa Russia na viongozi wa Afrika

Mwezi uliopita, Haji Abubaker Jeje Odongo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda alisema, nchi yake haitayumbishwa na mashinikizo yanayotolewa na wakoloni wa zamani katika nchi za Magharibi ya kuitaka iwe dhidi ya Russia, ikizingatiwa kuwa uhusiano wa muda mrefu wa pande mbili na Moscow ni muhimu sana kwa Kampala.

Uganda ilikuwa miongoni mwa mataifa kadhaa ya Kiafrika ambayo yaliamua kutopiga kura, wakati Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipopigia kura maazimio yaliyoandaliwa na nchi za Magharibi ili kuilaani Russia kuhusiana na mzozo wa Ukraine mwezi Machi na Oktoba mwaka jana.