Ripota Maalumu wa UN ataka kuwekewa vikwazo utawala wa Kizayuni
Ripota Maalumu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na suala la haki ya chakula ametaka kuwekewa vikwazo utawala wa Kizayuni kwa jinai unaozoendelea kutekeleza katika Ukanda wa Gaza.
Michael Fakhri amesema kuwa utawala wa Israel si tu unazuia kuingizwa misaada ya kibinadamu huko Gaza bali unaangamiza na kuharibu ardhi na miundo msingi ya chakula ya Wapalestina. Ripota Maalumu wa Umoja wa Mataifa anayehusika na suala la haki ya chakula pia ametaka kuwekewa vikwazo utawala wa Kizayuni na kutolewa mashinikizo dhidi ya waungaji mkono wa utawala huo.
Fakhri aliwahi kutangaza katika ripoti yake huko nyuma kwamba mwanzoni mwa mwezi Disemba mwaka jana Ukanda wa Gaza ulikuwa na asilimia 80 ya watu wanaokabiliwa na njaa duniani. Amesema, haijawahi kushuhudiwa katika historia ya vita mbalimbali duniani kuona raia wanataabika na kukabiliwa na njaa na ukosefu wa chakula kwa kiasi hicho.
Ripoti hii imetolewa katika hali ambayo Msemaji wa Umoja wa Mataifa Alhamisi iliyopita alisisitiza kuwa utawala wa Israel ambao ni dola vamizi huko Gaza unapasa kuhakikisha kuwa taasisi za masuala ya kibinadamu zinatekeleza vyema shughuli zao.
Stephane Dujarric amesisitiza kuhusu jukumu muhimu la Umoja wa Mataifa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Misaada kwa ajili ya Wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) kama uti wa mgongo na ufanikishaji misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza.
Wizara ya Afya ya Palestina imetangaza katika takwimu zake za karibuni kuwa hadi sasa karibu Wapalestina 41,000 wameuliwa shahidi na wengine zaidi ya 94,000 kujeruhiwa.