Iran: HAMAS ingali hai, itaendeleza njia yake kwa nguvu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla
(last modified 2024-10-20T07:07:16+00:00 )
Oct 20, 2024 07:07 UTC
  • Iran: HAMAS ingali hai, itaendeleza njia yake kwa nguvu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla

Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Sayyid Abbas Araghchi amesema Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS iko hai na itaendelea kufuata njia yake hiyo hiyo kwa nguvu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla licha ya kuuawa shahidi kiongozi wake Yahya Sinwar.

Araghchi, ambaye ameelekea Uturuki akiongoza ujumbe wa kidiplomasia kushiriki katika Jukwaa la Ushirikiano la Kikanda la 3+3 la Qafqazi Kusini linalofanyika mjini Istanbul, siku ya Jumamosi alikutana na kufanya mazungumzo na maafisa wakuu wa Hamas.
 
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya mkutano huo, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran alisema: "jambo moja ambalo ni muhimu kila mtu kulijua ni kwamba baada ya kuuawa shahidi Sinwar na (makamanda) wengine huko Ghaza, Hamas ingali iko hai na ni kitu halisi kilichopo Palestina ambacho hakuna mtu awezaye kukipuuza na kukitokomeza". 

Araghchi ameendelea kueleza kuwa, utawala ghasibu wa Israel umeshindwa kufikia malengo yake baada ya mwaka mmoja wa vita vya mauaji ya kimbari huko Ghaza, licha ya kufanya kila uwezalo na kuua zaidi ya watu 50,000, kuharibu nyumba nyingi na kufanya jinai nyingi zinazojulikana na kila mtu. 

Sayyid Abbas Araghchi (kulia) katika mazungumzo na  Mohamed Ismail Darwish 

Mwanadiplomasia huyo wa ngazi ya juu wa Iran amebainisha kuwa amefanya majadiliano ya kina na wajumbe wa ofisi ya kisiasa ya Hamas kuhusu vita katika Ukanda wa Ghaza, mazungumzo ya kusitisha mapigano pamoja na maudhui nyinginezo.

Amesema: "Hamas iko hai zaidi kuliko wakati wowote ule" na itaendelea na mikutano yake na nchi za eneo, na akasisitiza kwamba harakati hiyo ya Muqawamna "itaendelea kufuata njia yake kwa nguvu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo kabla".

Katika mazungumzo hayo na Mohamed Ismail Darwish, Mkuu wa Baraza la Shura ya Hamas, Araghchi amesema, ukatili mwingi ambao Israel imeufanya huko Ghaza katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita umeitia fedheha ya kudumu utawala huo ghasibu na waungaji mkono wake.

Aidha, amesema, hali mbaya ya Ghaza na Lebanon ni matokeo ya moja kwa moja ya "uungaji mkono haramu na usio na uwajibikaji" unaotolewa kwa utawala wa Israel na Marekani na madola mengine ya Magharibi.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran ameihakikishia harakati ya Hamas kwamba damu takasifu ya kiongozi wake Sinwar, na mashahidi wengine wa Muqawama itafungua njia ya kupata uhuru kamaili kutoka kwenye makucha ya ukaliaji ardhi kwa mabavu na ukandamizaji wa Israel.../

 

Tags