Ali Larijani: Maadui wanafanya njama za kuzusha mifarakano
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, katika mazingira ya hivi sasa katika Mashariki ya Kati kuna baadhi ya nchi ambazo mbali na kufanya uadui zinafanya kila ziwezalo kuzusha mifarakano katika eneo hili.
Dakta Ali Larijani alisema hayo jana alipokutana na kundi la watu waliojitolea katika vita vya kujihami kutakatifu wakati Iraq ilipoanzisha vita vya kichokozi dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kuongeza kuwa, Iran ina usalama mzuri mno katika Mashariki ya Kati.
Spika wa Majlisi ya Ushauri wa Kiislamu ya Iran amebainisha kwamba, madola ya Magharibi yamekiri mara chungu nzima juu ya Iran kuwa na usalama, amani na uthabiti miongoni mwa nchi za Mashariki ya Kati.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema bayana kwamba, katika mazingira ya sasa ya Mashariki ya Kati jambo lililo wazi ni kuwa, bila ya Iran amani ya eneo hili haiwezi kupatikana na kwamba, Marekani haiwezi kuthubutu kufanya shambulio lolote lile.
Spika Larijani ameeleza kuwa, moja ya yaliyokuwa malengo ya Iran ya kufanya mazungumzo na kufikia makubaliano ya nyuklia ni kuandaa mazingira na anga ya ustawi wa kiuchumi ambapo hivi sasa kuna mazingira yanayoandaliwa kwa ajili ya uwezekaji wa kiuchumi hapa nchini.